Tuesday, August 28, 2018

Shimo lililosababisha vifo vya watu 12 lazua mjadala bungeni

Shimo lililosababisha vifo vya watu 12 lazua mjadala bungeni


Dodoma/Tabora. Shimo lililosababisha ajali iliyoua watu 12 Igunga mkoani Tabora, limezua mjadala bungeni jana, huku waziri wa mambo ya ndani ya nchi, Dk Mwigulu Nchemba akiliagiza jeshi la polisi kuwaweka ndani madereva wanaoendesha kwa kasi.

Mjadala huo ulizuka, baada ya mbunge wa Ulanga, Mashariki (CCM) Goodluck Mlinga kuhoji kuhusu ajali hiyo iliyotokea juzi na kusema kuwa kama chanzo cha ajali hiyo ni ubovu wa barabara, basi Serikali haina budi kuitoza faini Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads).

Katika mwongozo wake, Mlinga alisema ajali hiyo imesababishwa na ubovu wa barabara na hivyo akataka Tanroads itozwe faini kama askari wa usalama barabarani wanavyowatoza madereva wazembe.

Ajali hiyo iliyotokea juzi, ilihusisha basi la abiria la City Boy na lori. Mbali ya kusababisha vifo hivyo vya watu 12, wengine 43 walijeruhiwa.

Hata hivyo, akijibu mwongozo huo, Waziri Nchemba alisema chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi lakini akaongeza kuwa lori ambalo ndilo lililosababisha ajali hiyo lilikuwa likikwepa shimo ndipo moja ya kifaa cha tairi kilipokakatika na kupoteza mwelekeo kisha kugonga basi.

�Kama jana nilivyosema kuwa tunapotoza faini lengo letu si kupata ile fedha, lakini lengo letu ni kuwakumbusha madereva kuwa wanatakiwa kutokwenda kwa mwendo wa kizembe na kasi unaoweza kusababisha madhara hayo,� alisema.

Alisema kutokana na watu kutozwa faini, wanachukulia adhabu hiyo kama mazoea na kudhani lengo ni kukusanya fedha wakati lengo ni kulinda usalama wao, �Naelekeza polisi watakapokamata dereva yeyote anayekwenda mwendo kasi pamoja na hiyo ya kuwatoza faini, wamuweke ndani hadi aende mahakamani. Kama rekodi yake ni mbaya, anyang�anywe leseni asiendelee kuendesha magari na kusababisha ajali.�

Wakati Dk Nchemba akisema hayo bungeni,
Rais Magufuli mbali na kutoa pole kutokana na ajali hiyo, amewataka viongozi wote wanaohusika na usimamizi wa usalama barabarani kutafakari kwa nini ajali nyingi zimekuwa zikitokea katika maeneo yaleyale na kutafuta ufumbuzi ili kuepusha madhara ya watu kupoteza maisha, kupata ulemavu wa kudumu na kupoteza mali.

Rais Magufuli katika taarifa yake iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa amesema, �Nimepokea kwa mshtuko na masikitiko makubwa taarifa za vifo vya watu 12 waliopoteza maisha katika ajali ya barabarani jana usiku (juzi) katika Wilaya ya Igunga mkoani Tabora, nawapa pole wafiwa wote, ndugu, jamaa na marafiki walioguswa na msiba huu mkubwa.

�Aidha, nalitaka Jeshi la Polisi, kamati za ulinzi na usalama za mikoa na wilaya na mamlaka zote zinazohusika na usalama wa barabarani kujitathmini na kutafuta majawabu ya kwa nini ajali za barabarani zinaendelea kutokea kwa kusababishwa na uzembe na uvunjaji wa sheria za barabarani.�

Kuhusu ajali hiyo, kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Wilbroad Mutafungwa alisema ilitokea baada ya lori lililokuwa likikwepa shimo kupasuka tairi hivyo dereva kushindwa kulimudu na kugongana uso kwa uso na basi kabla ya kupinduka.

Majeruhi wawili walipelekwa Hospitali ya Rufaa ya Bugando, Mwanza na mmoja alipelekwa Hospitali ya Nkinga na 43 walitibiwa katika Hospitali ya wilaya Igunga na miili sita kati ya 12, imetambuliwa na ndugu zao na mmoja wao ni mhasibu wa Halmashauri ya wilaya ya Igunga, Harold Nyamwangi.

SOMA PIA:18 Job Opportunities at The Tabora Urban Water Supply and Sanitation Authority

Mwananchi

go to link download

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.